Thursday 9 October 2014

KIJIJINI::WANAKIJIJI WACHEZA MUZIKI KUSHANGILIA UMEME

WAKAZI wa kijiji cha Mbegasera wilaya ya Kilosa mkoani Morogoro, wameshindwa kuzuia furaha yao na kuamua kusakata muziki baada ya umeme kufika kijijini hapo na wananchi kuunganishwa kwenye nyumba zao, ambazo walilazimika kuezua sehemu ya nyasi na kuezeka kwa bati ili kufungiwa nishati hiyo. 
 
Hayo yalionekana hivi karibuni wakati Watendaji wakuu wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA), walipotembelea maeneo mbalimbali nchini kuangalia utekelezaji wa miradi ya umeme vijijini wanayosimamia.
Msafara wa REA ulipopita kwenye kijiji hicho, ulishuhudia moja ya nyumba iliyoezekwa kwa nyasi na kuezuliwa sehemu kidogo na kisha kuezekwa kwa bati, ikiwa imeunganishwa umeme na unawaka, hivyo kuwafanya wanakijiji hao kuserebuka kwa kucheza.
"Tunacheza sisi tuna furaha ya umeme, hatukuwahi kuuona hapa kwetu, hadi uende mjini ndio kuna umeme, lakini sasa tunao acha tusarebuke, wala hatuleti ugomvi na mtu hapa", alisema Zanisha Kawaya mkazi wa eneo hilo.
Alisema wakati mradi huo unaanza kutekelezwa kijijini hapo, wananchi waliambiwa umuhimu wake na kuhamasishwa kujiandikisha kwa wale wanaotaka kufungiwa umeme, kwa kutoa shilingi 27,000 na mradi ulipokamilika walipata umeme.
Awali Mkurugenzi wa Huduma za Ufundi wa REA, Bengiel Msofe alisema hadi sasa wananchi 248 wa vijiji vinne vya wilaya ya Kilosa wameunganishiwa umeme kupitia mradi wa nishati vijijini, unaotekelezwa na wakala huyo.
Alisema lengo la kuwaunganisha wateja 300 wa vijiji hivyo vinne ambavyo ni Kisanga, Mbegasera, Msolwa na Kibaoni ambavyo wateja hao 300, wanaunganishiwa nishati hiyo kwa gharama ya bei ya ruzuku ya shilingi 27,000 tu badala ya ile ya kawaidia ya Sh 139,000.

No comments:

Post a Comment