Monday 18 August 2014

Rais Kikwete Amepoteza Dira......PROF:LIPUMBA

Lipumba: Rais Kikwete Amepoteza Dira

Monday, August 18, 2014
Profesa Lipumba alisema Rais Jakaya Kikwete ameshindwa kusimamia ahadi zake, hali inayochangia kupwaya kwa utawala wake.

Akifafanua hoja yake, mwanasiasa hiyo alisema, “Katika hotuba yake ya mwisho wa mwaka 2011 ambapo pia alianzisha mchakato wa Katiba, alisema kutakuwa na kituo cha kufua umeme cha megawati 300, kutakuwa na Kinyerezi (I) ya megawati 200, megawati nyingine 200 za makaa ya mawe na uzalishaji wa umeme kwa upepo.

“Hadi sasa imeshapita miezi 36, hakuna hata kimoja alichomaliza kukitekeleza, kituo cha kufua umeme cha Kinyerezi (I) kinaendelea kujengwa.”

“Kwa jumla, Kikwete ameshapoteza dira ya maendeleo kwa kipindi cha miaka tisa alichokaa madarakani, hivyo sioni cha kumshauri. Alisema tangu Kikwete aingie madarakani, hakuwa na ajenda maalumu ya maendeleo, ndiyo maana nchi imeendelea kuwa maskini.

“Kwa sasa, Rais Kikwete amebakiza muda wa mwaka mmoja, hakuna la kutegemea. Kwanza, hakuwa na mtazamo au dira ya kufanikisha mambo, kwa hiyo kwa mwaka huu mmoja huwezi kutegemea kuwa ataleta mabadiliko makubwa,” alisema Profesa Lipumba.

Profesa Lipumba, akirejea utawala wa kiongozi wa serikali ya awamu ya tatu, Benjamin Mkapa, alisema kuwa utawala wa Kikwete umeshindwa kuwa na nidhamu ya fedha kiasi cha kuzorotesha uchumi.

“Ili uweze kusimamia maendeleo ya nchi yetu, ni lazima uwe na matumizi mazuri ya fedha za umma na uwe na Serikali inayosimamia vizuri matumizi na malengo yaliyowekwa,” alisema msomi huyo wa nyanja ya uchumi.

“Rais Mkapa alikuwa na nidhamu ya utendaji wa Serikali kibajeti, kwa sababu alikuwa akitumia bajeti ya fedha taslimu. Ilitumika kuleta nidhamu kwa kuwa fedha zilizokuwapo, ndizo zilizotumiwa.

“Tatizo kubwa ambalo limejitokeza katika kipindi hiki… Bajeti kwa ujumla wake, ule mgawanyo wa kila wizara haukuwa na mwongozo mzuri wa nini Serikali itatekeleza. Tatizo hilo lilikuwa ni muhimu kwa awamu ya mwanzo kuleta nidhamu katika matumizi ya ujumla yalingane na mapato, lakini hilo jambo limeendelea mpaka leo.”

Chanzo: Mwananchi