Friday 22 August 2014

UCHAMBUZI WA LEO:IJUE CHUNYA NA UTAJIRI WAKE

SAUTI KUTOKA NYIKANI.... MULUGO, MWANASIASA MREFU KAMA UTAJIRI WA CHUNYA MBEYA

 
MBUNGE WA JIMBO LA SONGWE PHILLIPO MULUGO.


NA GORDON KALULUNGA
MWAKA 2011, Mwandishi Mubelwa Bandio, aliwahi kuandika kuwa, anatamani angekuwepo Mwalimu Julius Kambarage Nyerere ili ayaone yanayotendeka hivi sasa.
Alisema tamaa yake ni kuhusu uchumi wa dunia unakoelekea na namna mataifa yanavyochukua umiliki wa uendeshaji wa shughuli muhimu za kiuchumi kisha anaishia kujiuliza kama hii si sehemu ama aina mpya ya ujamaa?
“Kama Baba wa Taifa Mwl Nyerere angekuwepo, basi angeweza kurejea kusema mawili matatu ambayo alishawahi kusema miaka kadhaa iliyopita na ambayo yamekuwa katika hotuba zake na nukuhu zilizopo sehemu mbalimbali” anasema Mubelwa.
Anaendelea kwa kusema kuwa, anatamani angekuwepo akaona viongozi wetu wa sasa ambao hawawezi kusimamisha mapigano mpaka watishiwe na mataifa fulani, ama wawekewe vikwazo na fulani.
Katika andiko la makala yangu wiki iliyopita ukurasa huu, kuhusu baadhi ya wajumbe wa Bunge la katiba kutoka Chadema na kurejea Bungeni, lilileta maoni mengi na ninawashukuru wasomaji wote waliopiga simu na kutuma ujumbe mfupi wa maandishi.
Kabla ya Bunge hilo kuisha, nitaleta takwimu ambazo wengi hawataki kuzisikia ili mradi wahalalishe walichokisikia/wanachokitaka kuhusu serikali tatu, na hapo nitakumbusha neno “ukweli mchungu” la Mhariri wa Mtanzania Jumapili, Ratifa Baranyikwa.
Kwa leo sauti hii inatokea katika nyika ya wilaya ya Chunya mkoani Mbya.
Aliyekuwa Naibu waziri wa Elimu na mafunzo ya ufundi, Philipo Mullugo, kabla hajaangukiwa na jumba bovu la uteuzi mpya, alikuwa akionekana mchapa kazi na jambo hilo halina ubishi, labda ubishi uwe kwenye siasa chafu zinazoendelea kuishi hapa nchini.
Mulugo ni Mbunge wa Jimbo la Songwe, wilayani Chunya mkoani Mbeya. Mwonekano wake ni kiongozi kijana, umbile lake ni mwembamba na mrefu wa kutosha.
Katika wilaya hiyo ya Chunya kuna majimbo mawili ambayo ni Jimbo la Lupa linaloongozwa na Mbunge, Victor Mwambalaswa na linaloongozwa na Mulugo, liitwalo Jimbo la Songwe.
Historia inaonesha kuwa wilaya hiyo ndiyo wilaya kubwa kuliko zote nchini Tanzania.
Wilaya hiyo ina kilomita za mraba zipatazo 29,219 tarafa 4, kata 30 vijiji 73 na idadi ndogo ya watu wapatao 290,478.
Chunya ilianzishwa kwenye miaka ya 1948 na wakati huo ikiwa kama makao makuu ya wilaya ya Mbeya.
Wilaya hiyo ni moja kati ya wilaya za zamani au za mwanzo na zenye historia kubwa na ya pekee nchini.
Upekee wake unaazia kuwa ni wilaya ambayo imesahaulika kimaendeleo licha ya kuwa na rasilimali nyingi ikiwemo misitu ya mbao na dhahabu.
Enzi za ukoloni wakati nchi ikijulikana kwa jina la Tanganyika, waingereza walichagua wilaya ya Chunya kuwa makao makuu ya jeshi la polisi katika eneo la mgodi wa Saza(mine).
Sababu kubwa ya kuchagua eneo la mgodi wa Saza au Saza Mine kuwa makao makuu ya polisi katika koloni la Tanganyika ilikuwa ni kulinda maslahi ya dhahabu.
Sehemu nyingine za machimbo ya dhahabu katika wilaya hiyo zilikuwa zinasimamiwa na wakoloni, na maeneo hayo ni Chunya mjini, matundasi na Makongorosi.
Wilaya ya chunya imepata umaarufu wa kuwa eneo la kwanza hapa nchini kuleta wachimbaji madini katika maeneo ya Saza na Matundasi kutoka nchi za Northern Rhodesi kwa sasa Zambia na South Africa yaani Afrika kusini.
Enzi za ukoloni kabila wa wawemba kutoka Zambia na makaburu(Boers) kutoka Afrika kusini, ndiyo watu waliokuwa wakifanya kazi za migodini kwasababu walikuwa ndiyo wataalamu.
Utaalamu wao unaelezwa kuwa ulitokana na sababu kwamba nchi zao zilikuwa na migodi mingi ya shaba, dhahabu, Almasi na makaa ya mawe.
Hadi leo hii ukienda Matundasi, Chunya mjini na Saza utawakuta Wawemba wengi ambao zama hizo walitoka Zambia na kwa sasa wamebakia kuwa walowezi.
Marais wa zamani wa Afrika kusini Frederick deKlerk na Pietha Botha wote walizaliwa katika eneo la mgodi wa Saza wilayani Chunya kati ya miaka 1938 na kuendelea.
Viongozi hao mashuhuri baadaye walisoma shule katika sekondari ya Iyunga iliyopo Jijini Mbeya, ambayo zamani ilikuwa ikijulikana kwa jina la Mbeya European School(shule ya wazungu) kati ya miaka ya 50.
Rais wa Zamani wa Namibia Sam Nujoma na akina Thabo Mbeki, wamewahi kuishi Matundasi katika kambi ya wapigania uhuru iliyokuwa ikijulikana kwa jina la Tumbu.
Wilaya hiyo ya Chunya, ndiyo wilaya ya kwanza kuwa na kiwanja cha ndege na huduma za benki Tanzania, lakini mpaka sasa ni wilaya ya inayoonekana change kati ya wilaya tisa za mkoa wa Mbeya na wananchi kukosa huduma za kijamii.
Hapa hakuna mchawi, bali mchawi wa wilaya hiyo ni serikali yenyewe ambayo inaelezwa kuwa viongozi wengi wa nchi hii ama kwa kuingia ubia na makampuni ya watu wengine, wanaendelea kuila Chunya.
Wananufaika na rasilimali za wilaya hiyo hasa upande wa madini aina ya dhahabu na mbao za asili.
“Kuliwa” kwa Chunya hakujaanza leo, bali ni miaka mingi tangu enzi za Mwalimu Julius Kambarage Nyerere. Sauti hii ya nyikani, ndiyo maana imeamua kufananisha urefu wa Mbunge Mullugo na utajiri wa mkoa wa Mbeya, ambapo serikali ikiamua, wilaya ya Chunya itakuwa na maendeleo marefu kama alivyo Mullugo.
Mwandishi anapatikana kwa simu 0754 440749

No comments:

Post a Comment