Sunday 14 September 2014

AFYA::MAAMBUKIZI KATIKA NJIA YA MKOJO

Wiki iliyopita tulieleza kwa kina tatizo la maambukizi katika njia ya mkojo, leo tunaeleza dalili na tiba yake. Uwepo wa mawe katika figo na mirija ya figo hata ndani ya kibofu pia ni mojawapo ya chanzo cha maambukizi haya katika njia ya mkojo.
Dalili
Baadhi ya dalili za mtu kuambukizwa bakteria katika njia ya mkojo kubwa ni maumivu wakati wa kukojoa, mkojo kuwa na rangi ya njano kupindukia na kuwa na harufu kali japokuwa siyo kila mwenye dalili hizo ana maambukizi katika njia ya mkojo au wengine huita UTI yaani Urinary Tract Infection wana ugonjwa huu.
Dalili nyingine za maambukizi ni maumivu,  kutokwa na usaha au majimaji wakati wa kukojoa kabla au baada ya kukojoa kukiambatana na maumivu na kuhisi moto wakati wa kukojoa mkojo. Baadhi ya wanaume wakati mwingine hutokwa na majimaji katika njia ya mkojo wakati wa kujisaidia haja kubwa.
Wengine wenye maambukizi hujikuta wakipata vichomi katika njia ya mkojo, au kuhisi kuwashwa sehemu hiyo, kuumwa kiuno au tumbo na kadhalika.
Mgonjwa anaweza pia kukumbwa na homa kali mara kwa mara na mwili kuwa mchovu, kwa watoto hupoteza hamu ya kula na mwili kuonesha kuchoka. Wagonjwa wengine hupata maumivu kwenye kibofu cha mkojo ambapo husikia maumivu  ya chini ya tumbo usawa wa kitovu na huwa hayaishi.
Matatizo haya ya mfumo wa mkojo kama tulivyoona huko juu huwapata watu wote wanawake na wanaume.
Watu wenye  matatizo haya kila wakipima huambiwa wana UTI. Kwa wanaume huhisi hata nguvu za kiume kupungua na wanawake hupoteza hamu ya tendo la ndoa.
WAJAWAZITO
Kwa wajawazito ugonjwa unaweza kuhatarisha maisha yao na mtoto aliye tumboni. Bakteria wanaweza kuingilia mfumo wa damu na kwenda kusababisha madhara mengine kama vile  shinikizo la damu kuwa kubwa kwenye figo na hata kusababisha ufanyaji kazi mbovu wa figo.
TIBA
Maambukizi katika njia ya mkojo hutibika kwa dawa mbalimbali za kisasa baada ya kufanyiwa vipimo na kuthibitika kuwa mgonjwa ana maambukizi hayo.
Dawa ambazo anaweza kupewa ni kama vile Ciprofloxacin--, Fosfomycin, Monurol, Furadantin, Sulfam ethoxazole, co-trimax, ampicillin, gentamicin na kadhalika lakini asitumie dawa yoyote bila kupata ushauri wa daktari.
Ushauri
Tunashauri kwa mwanamke kwamba epuka kujisafisha sehemu za siri na maji yarukayo kwa kasi, pia epuka kupaka marashi sehemu hizo, ama kutumia pedi zenye kemikali ya kukata harufu kwani hizo huua bakteria wa asili wa ukeni hali ambayo hukaribisha bakteria wa maradhi kuzaliana kwa wingi.
Ujisafishapo baada ya kujisaidia anzia mbele kwenda nyuma kuepusha kuhamisha bakteria walio eneo la haja kubwa kuingia njia ya mkojo.
Kwa wale walio katika kipindi cha ukomo wa hedhi, wanaweza kushauriana na daktari juu ya kutumia aestrogen ya ukeni ili kuwasaidia kujikinga na maambukizi.Kwa mwanaume maambukizi haya huathiri nguvu za kiume na kujipenyeza hadi katika korodani na huathiri uzalishaji wa mbegu za kiume na kukufanya uwe mgumba.
Maambukizi ya njia ya mkojo huweza kusababisha matatizo ya tezi ya kiume (prostate), hivyo mgonjwa anatakiwa kumuona daktari.

No comments:

Post a Comment