Monday 20 October 2014

PEOPLE'S POWER:::CHADEMA YAFUNIKA IRINGA MJINI

Dk Slaa mbele ya wafuasi wa Chadema wa Iringa Mjini katika mkutano uliofanyika Mlendege mjini Iringa
Sehemu ya vijana waliohudhuria
Akisisitiza jambo
CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kimefanya mkutano katika uwanja mpana wa stendi ya mabasi ya Mlandege, mjini Iringa; mkutano uliolezwa na wapekuzi wa mambo ya siasa wa mjini hapa kwamba umevunja rekodi ya mikutano yote iliyowahi kufanywa na chama hicho mjini Iringa.
Kwa kadri muda ulivyokuwa unazidi kwenda wapenzi na wasio wapenzi wa chama hicho waliendelea kumiminika katika stendi hiyo na kusikiliza kile kilichohotubiwa na baadhi ya viongozi wakuu wa chama hicho.
Mbali na  Mbunge wa Jimbo la Iringa Mjini, Mchungaji Peter Msigwa, mkutano huo ulihutubiwa na Katibu Mkuu wake, Dk Wilbroad Slaa, Makamu Mwenyekiti Tanzania Bara, Profesa Abdalla Safari na Naibu Katibu Mkuu Zanzibar, Salum Mwalimu.
Wakati Mchungaji Msigwa alizungumzia mambo mbalimbali aliyofanya tangu alipochaguliwa kuwa mbunge wa Jimbo la Iringa Mjini mwaka  2010, wengine wote walizungumzia uchaguzi wa mwaka huu wa serikali za mitaa na vijiji, uchaguzi mkuu wa mwakani na dhamira ya vyama vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) kukubaliana kusimamisha mgombea mmoja mmoja katika chaguzi zote zajazo.
Katika mkutano huo, Dk Slaa aliwataka wafuasi wa chama hicho kwenda kwa wenyeviti wa mitaa na vijiji kwa lengo la kuandikishwa katika daftari la kuandikisha wakazi wa kila kaya ndani ya kata.
Daftari hilo kwa mujibu wa Dk Slaa ndilo litakalotumika kwajili ya uchaguzi wa Desemba mwaka huu wa serikali za mitaa na vijiji.
“Ni haki ya kila mtanzania kuandikishwa katika daftari hilo. Daftari hilo sio la CCM wala la chama chochote, ni kwa ajili ya watanzania wote, kwahiyo akikisheni mnaandikishwa ili muwez kushiriki katika uchaguzi huo,” alisema.
Aliwasihi wafuasi wa chama hicho kutopuuza suala hilo kwani wakianya hivyo nafasi yao ya kushinda katika uchaguzi huo itakuwa ndogo.
“Kwahiyo msije mkajitokeza kuilalamikia CCM baada ya kuangushwa katika uchaguzi huo,” alisema.
Kuhusu Katiba
Dk Slaa alisema Ukawa watapita mtaa kwa mtaa na kijiji kwa kijiji pindi Katiba inayopendekezwa itakapopelekwa kwa wananchi kwa ajili ya kupigiwa kura.
“Hata ikiletwa kesho, hatuna shida, lakini CCM ni lazima wajue kwamba tutapita kila mahali kwa lengo la kuwahamasisha wananchi kuikataa,” alisema na kuongeza kwamba wanaikataa kwa kuwa haitokani na mapendekezo ya wananchi.
Kuhusu Uchaguzi Mkuu wa mwakani
Dk Slaa alisema Ukawa wako katika hatua za mwisho za makubaliano ya kusimamisha mgombea mmoja mmoja katika chaguzi zote.
Hata hivyo alisema pamoja na makubaliano hayo kutakuwa na vigezo vitakavyotumiwa ili kuwapata wagombea safi .
“halitakuwa suala la kupeana tu, eti kwasababu tumekubaliana hivyo, ni lazima tupate wagombea wenye sifaili tuweze kukabiliana vizuri na CCM,” alisema.
Ili kufanikisha chaguzi hizo, chama hicho kilisema kinahitaji rasilimali fedha na ndipo ulipotolewa wito kwa wafuasi wake kuchangia kupitia mfumo wa simu za mkononi.
“Hatuhitaji fedha nyingi kutoka kwenu, tuchangieni Sh200, 300 au 500 ili zisaidia katika harakati za mabadiliko,” Dk Slaa alisema wakati Naibu Katibu Mkuu Zanzibar, Salum Mwalimu aliyewahi kufanya kazi na VODACOM akitoa maelezo ya namna ya kukichangia chama hicho kwa kutumia mitandao ya simu,” alisema.
Itaendelea……………………………………………………………….

No comments:

Post a Comment