Monday 20 October 2014

UCHAMBUZI WA KISIASA>>SAUTI YA NYIKANI..... MWAITELEKE, KIJANA MSOMI ANAYETAJWA MBIO ZA UBUNGE MBEYA MJINI


NA GORDON KALULUNGA
WIKI hii ni wiki ya Vijana, Rais Jakaya Kikwete, wakati anazima mwenge wa uhuru mkoani Tabora mwanzoni mwa wiki na kumbukumbu ya miaka 15 ya kifo cha Mwalimu Julius Nyerere, alisema vijana ndiyo wanufaika wakubwa na Tanzania ijayo.
Katibu Mkuu wa CCM Taifa, Abdulhaman Kinana, akiwa mjini Dodoma wakati wa semina za makatibu wa CCM nchi nzima katikati ya wiki hii, amewaambia kuwa katika ngazi zao za uteuzi wawe makini kupendekeza majina ya watu wanaokubalika na jamii badala ya fedha.
Ukitaka kuwaudhi baadhi ya viongozi wa CCM, ambao wamezoea kufikiri kidogo badala ya kufikiri sana, waulize swali la kwanini majimbo ya upinzani yanaongezeka.
Wanaishia kusema kuwa ni kutokana na makundi ndani ya chama, badala ya uhalisia kuwa rushwa katika ngazi za uteuzi imetawala, hivyo watu wanaokubalika katika jamii wasio na fedha huachwa.
Leo sauti ya nyikani inatokea mkoni Mbeya na kuangaza upepo wa kisiasa uliopo jimbo la Mbeya mjini.
Kwa sasa Jimbo la Mbeya Mjini lipo chini ya Chama cha demokrasia na Maendeleo(Chadema), na Mbunge wake ni Joseph Mbilinyi.
Mbunge huyu amekuwa akipongezwa na baadhi ya wananchi kuwaletea maendeleo katika kata zao kwa kile wachambuzi wa masuala ya siasa mkoani hapa wakisema anatumia vema hasa usimamizi mzuri wa matumizi ya fedha za mfuko wa Jimbo.
CCM, inahaha kulirejesha jimbo hilo katika himaya yake, lakini kitendawili kinabaki miongozi mwao kuwa ni nani mwenye kuwaunganisha wote, ukizingatia kuwa asilimia sabini ya wajumbe wa kamati ya siasa ambayo ni kikao cha maamuzi kwa watakaohitaji kugombea nafasi hiyo nao wanatajwa kuwemo kwenye mstari wa safari hiyo ya matumaini.
Baadhi ya watu wanaotajwa kuwemo katika kinyanganyilo hicho cha ubunge nje ya kamati ya siasa ya CCM wilaya ya Mbeya mjini ni pamoja na Mkurugenzi wa Shirika la nyumba Tanzania(NHC), Nehemiah Mchechu, Mwenyekiti wa saccos kubwa Jijini Mbeya, (UWAMU SACCOS), Rodrick Y. Nyaluke na mjasiliamali kijana, Nwaka Mwakisu.
Wengine ni Mkuu wa wilaya ya Newala, Christopher Magala na Mtaalamu wa Masuala ya Ufuatiliaji na Tathimini, Ofisi ya Waziri Mkuu – Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM – TAMISEMI), Eliurd Leonard Mwaiteleke.
Leo nikianza na kijana Eliurd Mwaiteleke, anatajwa katika mbio hizo za kuweza kupeperusha bendera za CCM katika jimbo hilo la Mbeya Mjini kwa nia ya kukomboa jimbo, huku baadhi ya vijana wakimpa ‘‘dole’’, ukizingatia kuwa ni kamanda wa UVCCM kata ya Sinde Jijini Mbeya na alipendekezwa kuwa kamanda wa UVCCM mkoa wa Mbeya, akuweza kufanikiwa kutokana na umri wake.
Kabla sijaandika makala haya, nilijaribu kumtafuta na kutaka kujua wasifu wake, mbali na kukataa kuwa ni mmoja wa waliotangaza nia katika jimbo hilo, alisema kuwa yeye ni mtoto wa masikini lakini jitihada zake zimemfikisha hapo alipo.
Mwaiteleke alizaliwa May 28, 1977,  eneo la Mwanjelwa jijini Mbeya, mwaka 1986 alipelekwa kujiunga na shule ya Msingi Salemu, wilayani Rungwe mkoani Mbeya na kuhitimu mwaka 1992, kisha akajiunga na shule ya sekondari Ivumwe Jijini Mbeya kati ya mwaka 1993-1996 na mwaka 1997 na 1999 akajiunga na kidato cha tano na sita shule ya Sekondari Malangali
 Kijana huyu, anasema kwa sasa ana elimu ya Shahada ya Uzamili katika Sayansi ya Maendeleo ya Sera (Master Degree of Science in Development Policy (MSc.DP), aliyotunukiwa katika Chuo Kikuu Mzumbe, baada ya kusoma tangu mwaka 2009 – 2011, akitokea Chuo Cha Mipango ya Maendeleo Vijijini (Institute of Rural Development Planning - Dodoma (IRDP) baada ya kuwa na cheti na stashahada ya juu katika masuala ya mipango na mazingira.
Kijana huyu pia ni mtaalam wa masuala ya Ukusanyaji Takwimu Muhimu za usafi wa Mazingira, mtambuzi wa walengwa wa njaa  na ugawaji wa chakula na mwibuaji na msimamizi wa miradi ya kijamii kwa jamii iliyoathirika na UKIMWI.
Mwaiteleke anaonesha hulka na akipendacho kuhusu mipango na masuala mengine muhimu ya  mwelekeo wake kuwa ni kuungana na vijana wenzake kusaidiana mambo ya maendeleo kwa kutumia ujuzi na elimu aliyonayo hasa kuelezana kuhusu fursa zilizopo, changamoto na namna ya kuzifikia pamoja na kuzitatua ili wapate maendeleo yanayotarajiwa.
Kuhusu heshima ya Mbeya anasema, ni vema vijana wa mkoa wa Mbeya, wakatambua namna wazee wao jinsi walivyojenga heshima ya Mkoa wa Mbeya na namna wao wanavyoweza kusaidia kurudisha heshima na hadhi ya Mbeya inayopotea siku hadi siku.
Anaamini katika juhudi kwa kila jambo ili kuweza kuleta tofauti katika maisha ya jamii nzima ya wana Mbeya, ikiwa ni pamoja na kuanzisha mijadala ya wazi kwa vijana katika Nyanja mbalimbali.
Nyanja ambazo anazipa kipaumbele katika mijadala ni pamoja na masuala ya maendeleo ya elimu (tathimini ya elimu katika mkoa), afya, Mazingira na usafi wa Jiji la Mbeya, ukuzaji kipato cha jiji na kuwafikia wananchi, Miradi ya maendeleo, fursa za mikopo kwa vijana na wanawake na namna ya kuzikifikia.
“Tulikuwa na viwanda Jijini Mbeya, leo hii vimepungua, ni suala ambalo pia linahitaji mijadala kwa ajili ya kujua namna vinavyoweza kutengeneza ajira kwa vijana, kuanisha mapungufu yanayokwamisha maendeleo ya Mkoa na Kuanisha mapungufu na changamoto zinazowakabili vijana” anasema Mwaiteleke.
Anasema angependa vijana wawe na mwanga wa kutambua masuala ya jiji , uwajibikaji wake pamoja na ubunifu wa kiutendaji, kujua kufanya mapitio ya mipango inayopangwa kila mwaka kama inaleta tija kwa kundi kubwa la vijana ama la.
Kwa upande wa mtazamo wake kuhusu wazee anasema ni muhimu kutambua mahitaji halisi ya wazee na vipaumbele vyao na jinsi ya kuwatekelezea mahitaji yao bila kusahau masuala ya akina mama na vipaumbele vyao.
Hasiti kueleza kuhusu masuala mtambuka ya VVU, kilimo na fursa ya kilimo cha maua kwa vijana hasa ukizingatia fursa ya uwanja wa ndege wa kimataifa wa Songwe na fursa za wasomi waliopo na wajasiliamali.
Huyu ndiye kijana Eliurd Mwaiteleke, ambaye anatajwa kuwa na nia ya kuipeperusha bendera ya CCM katika Jimbo la Mbeya Mjini kwa lengo la kulikomboa Jimbo kutoka mikononi mwa Chadema.
Wiki ijayo tutamwangalia kijana mjasiliamali na mpenda michezo kwa vijana wenzake Nwaka Mwakisu.

No comments:

Post a Comment