Friday 15 August 2014

UKATILI au KUKU NA MAYAI YAKE?ABAKWA NA BABAE NA UKIMWI JUU YAKE.

UKATILI: Mkasa wa Binti aliyebakwa na Baba yake na kuambukizwa UKIMWI

Udaku Specially on Sunday, June 2014
“Amini usiamini hizi ni zama za mwisho mwanangu, mimi hili suala bado haliniingii akilini kabisa, kwani nilizoea kusikia kama hadithi kuwa mzazi ana uhusiano wa mapenzi na mwanawe, lakini leo hii yamenikuta ya kunikuta,” haya ni maneno ya Bhoke Mwita (siyo jina halisi), mama mzazi wa binti anayedaiwa kubakwa na baba yake mzazi kwa miaka minne.

Bhoke anasema kibaya zaidi mwanaye  amefanyiwa unyama huo na baba yake mzazi, huku akimwachia doa ambalo haliwezi kufutika milele ambao ni ugonjwa wa Ukimwi.

Tukio hilo linamsababisha Wanjara kunyamaza kwanza kabla ya mahojiano, baadaye anadai binti yake kapewa ujauzito na maambukizi ya Ukimwi na baba yake, ingawa alikuwa hajitambua kuwa ni mgonjwa hatua ambayo imemuumiza na kumtia aibu kwenye jamii.

Binti anayedaiwa kubakwa na baba yake, kupewa ujauzito na kuambukizwa Ukimwi. Picha na Florence Focus.
Binti anayedaiwa kubakwa na baba yake, kupewa ujauzito na kuambukizwa Ukimwi. Picha na Florence Focus.
Mkazi huyo wa Mtaa wa Kigera Kibini, Kata ya Kigera, Manispaa ya Musoma mkoani Mara, anasimlia historia ya maisha yake hadi kuzaa mtoto huyo wa mwisho nje ya ndoa baada ya mumewe kufariki, lakini hatima imekuwa kugeuzwa mke mwenza.

Mwita anasita kuendelea na simlizi kabla binti yake aliyefanyiwa unyama na baba yake, hajasimulia masaibu yake: “Matatizo niliyonayo ni mengi, Mungu pekee ndiye anayefahamu, bado naongezewa msalaba mzito kama huu.”

Ghafla anapaza sauti anaita jina la binti yake aliyefanyiwa ukatili, aliyekuwa chumba kingine na kumtaka aeleze yote yaliyomsibu ili ulimwengu utambue.

Simulizi za binti

Anatokea binti mrembo ila sura yake inaonyesha unyonge, mrefu, mwembamba  anasalimia kwa sauti ya upole huku akielekea kwenye kiti kuketi, afya yake siyo ya kuridhisha.

Bila kupoteza muda, binti huyo anadai alianza kuishi na baba yake mwaka 2002  akiwa anaingia darasa la tatu, baada ya mama yake kupata kibarua kwenye  nyumba ya watawa.

Anasema baba yake alikuwa akiishi na kaka zake wawili wakubwa ambao walikuwa wamemaliza shule na wakati huo walikuwa wakijihusisha na kazi za vibarua.

Anasimulia kuwa alipofika darasa la tano, baba yake alikuwa akimfuata chumbani kabla ya kaka zake hawajarudi nyumbani na kumtaka afanye naye ngono.  Binti huyo anasema kwamba wakati huo alikuwa hafahamu chochote kuhusu mapenzi.

 “Nilipoona baba ananipiga kila siku, nilikubali, akawa anakuja chumbani kwangu na wakati mwingine ananiita kwake, tukishamaliza ananiambia niende kwangu kulala, hivyo nikaona kama jambo la kawaida,” anasimulia binti huyo.

Anaendelea kusema kuwa baada ya kumaliza shule ya msingi mwaka 2009, alibaki na jukumu la kumhudumia baba yake kama mume wake, jambo ambalo anadai  lilikuwa likimuumiza, hivyo akaamua kuwa wazi ili apate msaada.

“Mwaka 2010 nilikuwa tu nyumbani, kazi yangu ilikuwa kumhudumia baba, kupika na kuchota maji, marafiki zangu hawakuruhusiwa kufika nyumbani, pia sikutakiwa kutoka, nikizungumza na jirani baba anakuwa mkali kama mbogo, nikaamua kumshirikisha dada yangu (anamtaja) ili anisaidie, japo alikuwa akiniuliza kuhusu jambo hilo namkatalia,” anadai.

Baada ya kumweleza dada yake, alimpa mbinu za kutoroka ili amsaidie kumfikisha kwa mama yao aliyekuwa amehamia Kijiji cha Kabasa, Wilaya ya Bunda.

Mama mzazi anena

Bhoke anasema baada ya mumewe wa ndoa kufariki mwaka 1989, alianza uhusiano na mwanamume huyo (anamtaja) alipata mimba na kujifungua binti huyo Septemba 3, 1994.

“Nilipojifungua mwanamume huyo alinitunza vizuri, alimpenda mwanawe hivyo sikuhangaika kumlea ingawa alikuwa mume wa mtu, kwa sababu alikuwa na familia yake,” anasimlia Bhoke.

Anasema kuwa mwaka 2003 alipata kibarua cha upishi nyumba ya watawa wa Shirika la Utawa mjini hapa, huku akitakiwa kuishi kwenye nyumba hiyo hivyo ilimlazimu kumtafutia mtoto wake sehemu ya kuishi kutokana na nyumbani kwake kutokuwapo mtu.

Mama huyo anadai baada ya mwanamume kupata taarifa kuwa mtoto amepelekwa kuishi kwa babu yake, alimfuata na kumwomba ampe mwanaee akamlee.

“Sikuwa na sababu za kumnyima mtoto, kwani ni wake, hivyo nilimkabidhi. Hata hivyo, nyumbani kwake hapakuwa mbali na nilipokuwa naishi,” anasema Bhoke na kuongeza:

“Kipindi anamchukua alikuwa anaingia darasa la tatu, hivyo alikuwa na akili ya kutambua zuri na baya, niliamini kama ataona anateseka atarudi hapa kwa dada zake.”

Anasema yeye aliendelea kufanya kazi nyumba ya watawa kwa miaka miwili, kisha akarejea nyumbani na  kuamua  kwenda kijijini kulima.

Bhoke anadai kabla hajaenda kijijini alikuwa akisikia maneno kwa majirani kuwa, mzazi mwenzike ana uhusiano wa kimapenzi na binti yake, lakini hakuamini, huku akimtaka binti yake mmoja kufuatilia ukweli wa tetesi hizo.

Anadai mwaka 2007, binti yake alianza kutaja maovu ya baba yake kwa dada yake, lakini akimtaka asimweleze mama yake, ingawa alimwambia licha ya kusema kuwa baba yake akimtaka kimapenzi, hakutamka iwapo wanajamiiana.

“Baada ya kupata taarifa hizo nilianza kuhisi kitu ila sikuwa na la kufanya, kwa sababu mtoto mwenyewe hana ushirikiano wa kutosha,” anadai Bhoke.

Mwaka 2007, binti alimaliza elimu yake ya msingi Shule ya Kamnyonge lakini alishindwa kuendelea na sekondari.

Anadai baada kushindwa, baba yake alimpeleka Shule ya Msingi Nyasho kurudia  darasa la sita, hivyo alimaliza tena darasa la saba mwaka 2009 lakini hakufaulu.

Taarifa zilivyojulikana

Dada yake binti huyo anadai baada ya mdogo wake kukiri baba yake anajamiiana naye kwa lazima, alimhurumia na kumsihi atoroke na kwamba atampa nauli aende kwa mama yake kijijini. Anasema alipofika kwa mama yake alitafutiwa shule akarudia darasa la saba Shule ya Msingi Kung’ombe, Wilaya ya Bunda mwaka 2011, alifaulu na kujiunga na Sekondari ya Wariku mwaka 2012.

Anadai baada ya kufunga shule Juni akiwa kidato cha pili, alimlazimisha mama yake ampe nauli ili aende Musoma kumsalimia baba yake. Anadai alipofika kwa baba yake hakurejea tena Bunda, zaidi ya baba yake kumpigia simu mama yake kuwa mtoto wake anateseka hivyo anamchukulia uhamisho asomee Musoma Mjini.

Anadai mdogo wake alihamia Sekondari ya Nyasho mjini hapa, ambako alisoma miezi miwili na kuachishwa na baba yake na kumpeleka Kijiji cha Sirorisimba, wilayani Serengeti kufanya kazi za hotelini.

Hata hivyo, anadai siri ilifichuka baadaye kwamba mdogo wake alitoroshwa  kutokana na ujauzito, hivyo baada ya mimba kukua alishindwa kuendelea na kazi ili apate nauli ya kurejea kwa mama yake Bunda.

Baada ya kufika kwa mama yake, alimpeleka kupima ingawa binti huyo alikataa kuwa siyo mjamzito lakini vipimo vilionyesha ana ujauzito.

Mama yake alimpa nauli ya kurudi kwa baba yake kwa sababu alimchukua kwa madai ya kumsomesha, hivyo hakuona umuhimu wa kumpokea akiwa na hali hiyo.

Dada yake anaendelea kusema, siku moja alikwenda kumsalimia mdogo wake na kumkuta akiwa na hali mbaya, hatua iliyomshtua na kumpigia simu mama yao  na ndugu zake wengine ili kumpa msaada wa kumpeleka hospitali.

“Nilimkuta mdogo wangu akiwa na hali ambayo siyo nzuri kwa kweli, alikuwa kavimba mwili mzima, halafu amejisaidia haja kubwa na ndogo hapohapo kitandani hakuna msaada, niliumia sana!”

Baada ya kumpeleka hospitali vipimo vilionyesha ana maambukizi ya virusi vya Ukimwi, walimpa ushauri nasaha na kumwanzishia dawa za kuzuia maambukizi ya mama kwenda kwa mtoto.

Anasema binti alikaa nyumbani wiki moja tu na kujifungua mtoto akiwa amekufa, kufuatia hali hiyo taarifa zililifikia Dawati la Jinsia la Polisi na kumtia mbaroni mtuhumiwa.

Msaada wa kisheria

Awali, binti huyo alikuwa akipewa msaada na Shirika lisilo la Serikali  la Watoto Wapinge Ukimwi (WWU) mjini hapa kama mtoto anayeishi katika mazingira magumu, walimsaidia akiwa darasa la kwanza hadi la saba, baada kuhitimu elimu ya msingi hawakuendelea naye.

Mkurugenzi wa shirika hilo, Sista Marion Haqhes anasema hawezi kumzungumzia mtoto huyo kwa sababu shirika lake na sheria ya mtoto haimruhusu ingawa tukio hilo ni kweli.

Polisi wanena

Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mara, Paul Kasabago anathibitisha kuwapo taarifa za ubakaji na kwamba, mtuhumiwa amekuwa akimbaka binti yake muda mrefu.

Kasabango anasema licha ya mtuhumiwa kumbaka binti yake mara kwa mara, amemsababishia ujauzito aliojifungua mtoto aliyekufa na vipimo vimeonyesha amemwambukiza Ukimwi.

Anasema kwa sasa mtuhumiwa yupo rumande kwa mahojiano zaidi na kwamba, atafikishwa mahakamani muda wowote.