Tuesday 9 September 2014

HAYA NDO MADHARA YA KULA CHIPS KWA AFYA YAKO


Kama moja ya njia ya kupunguza gharama za matumizi, watu wengi wanatumia mafuta yaleyale zaidi ya mara moja kukaangia vyakula mbalimbali.

Jambo hili linafanywa sehemu mbalimbali kama vile nyumbani, migahawani, hotelini, shuleni na zaidi mitaani kwa wakaanga shipsi, mihogo, mandazi, samaki na kitimoto.

Watu wanaotumia mafuta zaidi ya mara moja inawezekana wanafuata mazoea na kijamii lakini kwa kujua ama kutojua hatari za hulka hiyo kiafya.

Mtu anavyotumia mafuta zaidi ya mara moja, ubora wa mafuta hayo unapungua. Mafuta yenye ubora mdogo yakitumika kukaangia vyakula yananyonywa mengi katika vyakula.

Mtu akila vyakula hivyo atapata uzito kupita kiasi, lehemu kwa wingi na shinikizo la damu. Vitu ambavyo vyote vinachochea ugonjwa wa kisukari na magonjwa ya moyo.   Zaidi ya hayo, mafuta yaliyotumika kukaangia vyakula huwa yana mabaki ya vyakula. Mafuta hayo yakipoa vijidudu vya bakteria watakula mabaki hayo na kuzaliana kwa wingi.

Mafuta yenye mabaki ya vyakula yanapokosa hewa huwa yanaweza kuwa na mazingira mazuri ya bakteria aina ya “Clostridium botulinum” kuzaliana.

Bakteria wa aina hiyo anasababisha ugonjwa hatari unaotokana na ulaji wa vyakula vyenye sumu unaoitwa “botulism”.

Kuyahifadhi mafuta katika friji au friza unapunguza bakteria kuzaliana. Lakini watu wa namna hiyo kwenye jamii huwa wanayahifadhi tena wakati mwingine kwenye mazingira machafu.

Mtu anavyotumia mafuta kukaanga vyakula zaidi ya mara moja, uwezo wa mafuta hayo kuhimili joto unapungua na yanaweza kuzalisha kemikali kama vile zinazoitwa “freeradicals” ambazo zinaweza kuharibu ubora wa chakula na kuharibu chembehai na kuongeza uwezekano wa mtu kupata ugonjwa wa saratani.  Mafuta yanayotokana na mimea yanahimili zaidi joto wakati wa kukaanga vyakula kuliko yale yanayotokana na wanyama.

Mafuta yaliyosafishwa pia, yanahimili zaidi joto kuliko yale yasiyosafishwa. Mafuta ya aina hiyo ndiyo yatumike.

Mafuta yaliyosafishwa ya zaituni (olive), jamii ya karanga, soya na alizeti ni miongoni mwa yale yenye uwezo mkubwa wa kuhimili joto kali na hivyo ni mazuri kwa matumizi ya kukaangia vyakula.

Kwa usalama wa afya na ubora wa vyakula vitakavyo kaangwa, watu wanashauriwa kutumia mafuta mapya kila wakati wanapokaanga vyakula.

Hata hivyo, uzoefu unatuonyesha kuwa kwa watu wanaokaanga kiasi kikubwa cha vyakula ndani ya chombo chenye mafuta mengi, siyo rahisi kila wakati kutumia mafuta mapya kwani ni gharama na inaweza kusababisha hasara.

Mafuta yanaweza kutumika zaidi ya mara moja kukaangia kwa masharti yafuatayo. Mtu anapokaanga vyakula asitumie moto mkali sana kwa sababu utaharibu mafuta na chakula anachokiandaa.

Hii haina maana kuwa atumie moto mdogo kiasi ambacho chakula hakitaiva na kushindwa kuua vijijidudu vilivyomo katika vyakula vibichi.

Mtu asichanganye mafuta mapya na yale yaliyotumika. Vyakula visiwekwe chumvi nyingi ili kulinda nguvu ya mafuta kuhimili moto.

Mafuta yakipoa, yachujwe haraka kwa kutumia kitambaa safi ili kuondoa mabaki ya vyakula. Mafuta yafunikwe na kuhifadhiwa katika chombo safi.

No comments:

Post a Comment