Monday 27 October 2014

BURUDANI>>JOKATE: HAKUNA KAMA DIAMOND

Stori: Waandishi Wetu
Jumamosi iliyopita, Oktoba 25, 2014 ilikuwa ni Siku ya Msanii Duniani ambayo kwa mara ya kwanza, Tanzania iliiadhimisha siku hiyo katika Ukumbi wa Mlimani City jijini Dar, mgeni rasmi akiwa ni Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Gharib Bilal.
Dr Chris Mauki na Jokate Mwegelo walikuwa washehereshaji wa tamasha hilo kwenye Ukumbi wa Mlimani City uliopo Dar es Salaam.
Siku hiyo ilipambwa na matukio kibao nyuma na mbele ya pazia, ambapo kubwa lilikuwa ni la Jokate Mwegelo ambaye alikuwa miongoni mwa ma-mc wa shughuli hiyo ya kitaifa, kumfagilia waziwazi msanii Nasibu Abdul ‘Diamond Platnumz’, kwamba hakuna kama yeye, Ijumaa Wikienda lilikuwa ndani ya nyumba na kunasa matukio lukuki yaliyojiri.

Mc Jokate Mwengelo (kulia) akikata mauno baada ya burudani kumnogea.
SHUGHULI YAANZA
Kwa kuzingatia itifaki, ukiacha waalikwa wengine, kiongozi aliyeanza kutimba alikuwa ni Naibu Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Juma Nkamia na baadaye alifuatiwa na Dk. Bilal ambapo shughuli hiyo ilifunguliwa rasmi.
Kikundi cha ngoma za kinyeji kikitoa burudanu usiku huu Siku ya Msanii Mlimani City.
MA-MC
Washereheshaji wa shughuli hiyo walikuwa ni Chriss Mauki na Jokate Mwegelo ambao walifanya vizuri lakini mwanzoni kidizaini f’lani Jokate alionekana kuwa na kigugumizi na baadaye akatengeneza vichwa vya habari kufuatia kitendo chake cha kumsifia Diamond.
BURUDANI ZA AWALI
Katika burudani za mwanzo, kulikuwa na vikundi vya kudansi kisha ngoma ya asili kutoka Ukerewe ikafuatia, baadaye ikaja Bendi ya Mashauzi Classic chini ya Aisha Ramadhan ‘Isha Mashauzi’ ambayo haikuamsha kama ilivyozoeleka.
Staa wa Bongo Fleva, Nasibu Abdul 'Diamond Platnumz' akifanya yake.
TUZO ZAANZA KUTOLEWA
Tuzo ya kwanza kutolewa ilikuwa ni ya Msanii Aliyejitolea Maisha yake Yote Katika Sanaa ambayo ilikwenda kwa mchora katuni mahiri aliyechora michoro ya Tingatinga.
Tuzo ya pili ilikwenda kwa Msanii Aliyetoa Mchango Mkubwa kwa Jamii ambapo aliyeibuka kidedea ni Joseph Kanuti.
BURUDANI TENA
Baada ya tuzo hizo mbili, burudani iliendelea tena ambapo Ako Mpiluka Band walionesha mbwembwe za kucheza na moto na kuwakosha mashabiki waliohudhuria.
Diamond Akicheza na wanenguaji wake.
DIAMOND STEJINI
Baada ya Mpiluka Band, staa wa Bongo Fleva, Diamond Platnumz alitimba stejini ambapo aliangusha bonge la shoo mbele ya makamu wa rais na kushangiliwa.
Wakiendelea kucheza wimbo wa 'Mdogomdogo'.
Huku Diamond akiimba nyimbo zake nyingi za zamani, zile zomeazomea kama zilizotokea Fiesta zilizodaiwa kuwa ni kutoka kwa ‘Team Ali Kiba’, zilizimwa na uwepo wa makamu wa rais aliyeonekana kumkubali msanii huyo kwa kutingisha kichwa wakati anafanya shoo na sapoti kubwa aliyoipata kutoka kwa Jokate aliyeimba naye Wimbo wa Nimpende Nani.
Isha Mashauzi akifanya yake na wacheza shoo wake.
JOKATE: HAKUNA KAMA DIAMOND
Katika hali ambayo haikutarajiwa na wengi, Jokate alimfagilia waziwazi Diamond na kusema hakuna msanii anayeweza kumiliki jukwaa kama yeye.Sifa hizo alizozitoa Jokate kwa Diamond, zilisababisha ukumbi mzima ulipuke kwa kelele hasa ukizingatia kuwa wawili hao walishawahi kuwa wapenzi ila wakatengana na kile kinachodaiwa kuwa ni maneno ya watu.
Ukichanganya na kilichotokea kwenye Serengeti Fiesta 2014 ambapo Diamond ‘alikula za uso’ ukilinganisha na mpinzani wake, Ali Kiba ambaye alishangiliwa kwa nguvu, kitendo cha Jokate kumnadi Diamond jukwaani kilizidi kutengeneza vichwa vya habari.
DIAMOND ASAFISHA NYOTA
Baadaye Diamond aliangusha Number One na Mdogomdogo ambazo ziliwafanya watu wachizike hivyo kudaiwa kusafisha nyota yake iliyochafuka hivi karibuni kwenye Tamasha la Fiesta katika Viwanja vya Leaders Club, Kinondoni jijini Dar alipozomewa.
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mohammed Gharib Bilal akiongea jambo usiku wa kuamkia jana Mlimani City katika Siku ya Msanii.
DK BILAL AONDOKA
Baada ya neno kutoka kwa waandaaji, Waziri Nkamia alimuaga Dk. Bilal ambaye aliondoka ukumbini humo baada ya kukabidhi kitita cha Sh. milioni tano kwa kila mshindi wa tuzo mbili zilizotolewa.
Naibu Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo Mheshimiwa Juma Nkamia akiongea na wasanii katika Siku ya Msanii.
NJENJE WAKONGA NYOYO
Baada ya Dk. Bilal kusepa, burudani iliendelea ambapo Kilimanjaro Band ‘Wananjenje’ walikamatia jukwaa na kukonga vilivyo nyoyo za wahudhuria.
Waimbaji wanaounda kundi la Yamoto Band Aslay, Becka, Bella na Maromboso wakitoa burudani.
JOKATE AKATA MAUNO
Katika shoo ya Njenje, mwimbaji wake mashuhuri, Nyota Waziri alikuwa akitembea ukumbini kuwakatisha mauno wahudhuriaji na kuwataka wataje mahali wanakotokea  ambapo alipofika kwa Jokate, staa huyo alionesha umahiri mkubwa wa kukata mauno huku akijinadi kwamba anatokea Songea.
KOMEDI KUTOKA NAIROBI
Kilichofuata baadaye ni Kundi la The Omonds kutoka Nairobi, Kenya kupanda jukwaani na kuangusha komedi zilizowavunja mbavu wengi.
Baadaaye, ma-mc, Mauki na Jokate walipata nafasi ya kuzungumza chochote kabla ya kuwakaribisha Yamoto Band waliomaliza shughuli hiyo kwa kukamua ngoma zao kali zinazokimbiza mtaani kwa sasa.
Kwa picha zaidi angalia Uk. 8.
Imeandaliwa na Erick Evarist, Musa Mateja, Andrew Carlos, Nicolaus Trac na Dennis Mtima.

No comments:

Post a Comment