Friday 10 October 2014

KIGOMA>>MWANAFUNZI AFARIKI AKISAKA MAEMBE

MWANAFUNZI Hamimu Mussa (11), wa Shule ya Msingi Uhuru  Manispaa ya Kigoma Ujiji, amefariki dunia baada ya kuanguka kwenye mti wa mwembe na mwingine kuvunjika mguu na mkono.
Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake jana, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kigoma, Kamishna Msaidizi (ACP), Japhari Muhamed, alisema tukio hilo lilitokea juzi majira ya saa 10 jioni wakati wanafunzi wakiwa mapumziko, ambako wawili hao walipanda juu ya mwembe kwa lengo la kutafuta maembe.
Alisema kuwa wakati wanafunzi hao wakiwa juu ya mwembe, ghafla walianguka wote na Hamimu kupasuka kichwa na kufariki papo hapo, huku Baraka Ramadhani akivunjika mkono na mguu.
“Mti waliokuwa wameupanda ni mkubwa na mrefu, hivyo walikuwa mbali sana na ndio maana walipoanguka mmoja akafariki na mwingine kuvunjika,” alisema Kamanda Muhamed.
Alisema kuwa mwili wa marehemu tayari umeshakabidhiwa kwa ndugu zake kwa ajili ya taratibu za mazishi, wakati majeruhi amelazwa hospitali ya Mkoa Maweni kwa matibabu.
Kamanda Muhamed, amewataka walimu na wazazi kwa ujumla kuwa waangalifu kwa wanafunzi ili kuwaepusha na michezo ambayo ni hatarishi kwa maisha yao.

No comments:

Post a Comment