Wednesday 15 October 2014

USHAURI WA NDOA::MAUMIVU UNAPOFANYA TENDO LA NDOA (DYSPAREUNIA)

Tatizo hili huwasumbua baadhi ya wanawake walio katika umri wa kuzaa, yaani kuanzia miaka 18 hadi 40. Tatizo huweza kuanza ghafla au taratibu pale mwanamke anapofanya tendo.
Maumivu haya hutokana na hali ya mabadiliko ukeni ambapo uke huwa mkavu daima au mwanamke anapata vipindi vya ukavu ukeni na katika mlango wa kizazi pia husababisha tatizo hili.
Maumivu yanaweza kuwa ndani ya kizazi, yaani wakati wa tendo unahisi kuna kitu kinasukumwa na ukahisi maumivu ya tumbo chini ya kitovu na kiuno wakati wa tendo.
Maumivu pia yanaweza kutokea baada ya tendo la ndoa, mwanamke akafanya tendo la ndoa vizuri lakini anapomaliza tu akijigeuza anahisi maumivu chini ya kitovu na kiuno na wakati mwingine hata kichefuchefu.
Chanzo cha tatizo
Tumeona vyanzo vitatu vya maumivu wakati wa tendo ambavyo ni ukavu ukeni. Huu unatokana na maandalizi hafifu kabla ya tendo. Endapo hakuna maandalizi yoyote basi uke unakuwa mkavu na unashindwa kufanya tendo au linafanyika kwa nguvu.
Ukavu unaweza kusababishwa na kutokuwa na hamu ya tendo au kutojisikia kufanya tendo, hili linaweza kusababishwa na matatizo ya kisaikolojia au katika mfumo wa homoni.
Michubuko ukeni na katika mdomo wa kizazi husababishwa na maambukizi, kansa au kufanya tendo la ndoa kwa nguvu bila maandalizi au ubakaji.
Maambukizi ukeni huambatana na kutokwa na uchafu wenye harufu na muwasho. Maambukizi yanaweza kusababishwa na fangasi, bakteria na magonjwa ya zinaa.
Maumivu ya ndani hutokana na maambukizi katika viungo vya uzazi mfano, ndani ya kizazi, mirija na vifuko vya mayai.
Maambukizi haya huanzia ukeni na kusambaa hadi ndani ya kizazi, lakini pia yanaweza kuanzia kwa ndani hasa baada ya kuharibika au kutoa mimba.
Dalili za tatizo
Maumivu wakati wa tendo la ndoa yanaweza kuanza mara tu tendo linapoanza, au tendo linapoendelea. Vilevile maumivu yanaweza kutokea baada ya tendo kumalizika.
Mwanaume pia anaweza kupata maumivu wakati wa tendo au baada ya tendo kutokana na michubuko katika uume, matatizo katika misuli ya uume, maambukizi ndani ya njia ya mkojo na matatizo ya korodani.
Maumivu ya kiuno kwa wanaume na wanawake pia ni mojawapo ya tatizo kubwa.
Uchunguzi
Tatizo hili la maumivu wakati wa tendo la ndoa huchunguzwa hospitali ambapo vipimo mbalimbali hufanyika kadiri daktari atakavyoona inafaa. Vipimo vya kuangalia ukeni, damu, mkojo na Ultrasound hufanyika kutegemea na ukubwa wa tatizo.
Ushauri
Ni vema uwahi hospitali kwa uchunguzi wa kina na tiba. Tatizo likiwa sugu yaani kukusumbua mara kwa mara husababisha upotevu wa hamu na raha ya tendo.
Kwa mwanaume hata uwezo wa kufanya tendo la ndoa hupotea. Waone madaktari katika hospitali ya mkoa na wilaya kwa uchunguzi na tiba.

No comments:

Post a Comment