Wednesday 15 October 2014

SAIASA::Kinana awaasa makatibu wa CCM wa wilaya na mikoa


 
Joyce Kasiki, Dodoma

KATIBU mkuu wa Chama Cha Mapinduzi Abdulrahaman Kinana amewaomba  makatibu wa CCM wa wilaya na mikoa nchini kufanya maandalizi mazuri kwa kuteua wagombea wazuri wanaokubalika,wanaopendwa na wanaoheshimika  katika jamii ili chama kiweze kushinda kwa kishindo katika chaguzi zijazo.

Kinana  alisema  hayo  mjini Dodoma wakati akifunga semina ya siku ya moja ya sekretarieti ya Halmashauri Kuu ya Taifa na makatibu hao.

Alisema kuwa, tukishinda vizuri kwenye uchaguzi wa serikali za mitaa watakuwa wamejenga msingi mzuri kwa ajili ya uchaguzi mwaka ujao ambapo ushindi huo huo utasaidia ushindi mwingine mkubwa zaidi wa madiwani,wabunge na rais mwaka ujao.

Vile vile alisema ,  yeye binafsi anaamini mwaka ujao pia ushindi ni kwa CCM kutokana na kazi nzuri inayofanywa na watendaji na viongozi wa chama na kuwaomba kujtahidi kadri ya uwezo wao kuongeza juhudi maarifa na ufanisi.

Kinana alisema   kuwa mwaka 2009 katika uchaguzi wa seriklai za mitaa ushindi wa CCM ulikuwa ni kwa asilimia 96 ambapo asilimia 4 zilizobaki waligawana vyama vya upinzani kama sehemu ya wao kupumulia hivyo anaamini hawatapata asilimia zaidi ya hizo walizopata.

Akielezea kuhusu ziara zake anazozifanya katika mikoa mbalimbali hapa nchini amesema ameridhishwa na maandalizi yaliyopo mikoani na wilayani hivyo hana sababu ya kutokuwa na imani kwamba ushindi kwa CCM utakuwa mkubwa sana.

Amesema mpaka sasa imebaki mikoa 8 ambapo mpaka mwezi februari mwakani atakuwa amemaliza mikoa yote nchini lengo likiwa ni kuimarisha chama, kusukuma,kusimamia, kuhimiza utekelezaji wa ilani na  ushindi katika uchaguzi wa serikali za mitaa na uchaguzi mkuu.

No comments:

Post a Comment