Wednesday 15 October 2014

UREMBO::USHINDI MTOTO WA MBUNGE, MISS TANZANIA YATIKISIKA

Stori:  Erick Evarist na Musa Mateja
OHOOOOH! Siku chache baada ya mtoto wa Mbunge wa Temeke, Abbas Mtemvu, Sitti kujinyakulia U-Miss Tanzania 2014, tayari joto la ushindi huo limetikisa taji hilo na kuibua maswali ‘chungu mbovu’ kuhoji uhalali wa ushindi huo, Risasi Mchanganyiko linashuka na mchongo kamili.
Miss Tanzania Sitti Mtemvu akiwa mwenye nyuso ya furaha baada ya kushinda taji hilo.
Kwa mujibu wa chanzo chetu, vuguvugu za uhalali wa ushindi ziliibuka muda mchache kabla ya shindano hilo kuchukua nafasi katika Ukumbi wa Mlimani City, Ijumaa iliyopita ambapo wadau mbalimbali walianza kuhoji kulikoni wafuasi wa mrembo huyo waingie na vipeperushi vingi vyenye picha ya mshindi (Sitti).
“Tatizo lilianzia kwa watu wengi kuingia na vibendera vyenye picha ya Sitti vikionyesha dhahiri kwamba walijua kabla kwamba ni mshindi hivyo kuja wakiwa wamejipanga kabisa,” kilisema chanzo.
Chanzo hicho kilienda mbali zaidi kwa kusema hata katika suala zima la mshindi kuandaliwa gari maalum la Hammer ambalo baadaye lilimchukua na kumrudisha kivyake tofauti na washiriki wengine ambao waliondoka ukumbini hapo na basi waliloandaliwa.
Miss Tanzania aliyemaliza muda wake,Happiness Watimanywa akimvika Crown na Taji Miss Tanzania Sitti Mtemvu.
“Waandaaji wanapaswa kutueleza vizuri, haiwezekani watu waandae Hammer waje nalo ukumbini pasipo kuwa na uhakika wa ushindi, ule ni utani,” kilinyetisha chanzo hicho.
Aidha, vuguvugu hilo lilijiongeza zaidi baada ya watu kudai huenda ushindi huo ulitokana na mgongo wa baba yake (mbunge wa Temeke) madai ambayo kwa pamoja yalikanushwa na muandaji wa mashindano hayo, Hashimu Lundenga.
“Hakuna kitu kama hicho, malalamiko kila siku hayakosekani, vipeperushi havikatazwi, majaji sita kati ya tisa waliwekwa na wadhamini (TBL kupitia kinywaji chao cha Red’s), haiwezekani akawahonga majaji wote hao.
“Kuhusu gari, hakuondoka ukumbini na Hammer, aliondoka na basi kama washiriki wengine, sijui hayo maneno yanatoka wapi,” alisema Lundenga.
Kwenye shindano hilo, Sitti aliwagaragaza washiriki wenzake 29 na kuondoka na kitita cha shilingi milioni 18. Mrembo huyo ndiye atakayeiwakilisha Tanzania katika mashindano ya dunia (Miss World) hapo baadaye.

No comments:

Post a Comment