Friday 15 August 2014

MAPENDEKEZO YA NYALALI HAYAKUTOKANA NA WANANCHI

                                                    

                                   UONGOZI WETU NA HATIMA YA   TANZANIA
Na. Julius Kambarage Nyerere
TOLEO LA KIZAZI KIPYA
2010

                                                       SURA YA KWANZA
             MAPENDEKEZO YA NYALALI HAYAKUTOKANA NA WANANCHI
Jambo la kwanza ambalo lilimsumbua Mwalimu ni jinsi gani hoja ya Tanganyika ilivyoletwa na kufikia
ilipofikia. Mwalimu aliona hoja hii wala isingekuwa na nafasi kama viongozi wangeweza
kuishughulikia mara moja kwa kutoa majibu ambayo ni ya kihistoria na ya kimantiki. Aliweza
kuthibitisha kwa vielelezo kuwa hoja ya Tanganyika haikutokana na mapendekezo ya wananchi bali
tume ya Jaji Nyalali ilionelea ni bora kutoa pendekezo hilo. Kwa Mwalimu, CCM tayari ilikuwa na
majibu yake kuhusu suala la serikali tatu, kwamba sera ya CCM ni serikali mbili na sababu zake
zilikuwa zinajulikana. Kitendo cha uongozi wa Chama na serikali kuliendeleza suala hili hadi kufikia
Bunge kutoa Azimio la kuundwa kwa serikali ya Tanganyika ndani ya “Muungano” kilikuwa ni kitendo
kilichoonesha uwezo mdogo wa kuhimili vishindo, uongozi duni, na utetezi dhaifu kabisa wa sera za
chama. Nyerere alijikuta ni mtu pekee ambaye yuko tayari kusimamia kanuni bila ya kujali gharama
au kuangalia sura za watu. Alinyosha mkono juu tayari kuhesabiwa – M. M.

                            1. RIPOTI YA JAJI NYALALI:
Tume ya Jaji Nyalali ilipendekeza mambo mengi, lakini yanayotuhusu hapa ni mawili:
(i) Pendekezo la kugeuza mfumo wa Chama Kimoja cha Siasa, na kuleta mfumo wa vyama vingi; na
(ii) Pendekezo la kugeuza mfumo wa Muungano wa Serikali Mbili, na kuleta mfumo wa Shirikisho la
Serikali Tatu.
La kwanza lilikubaliwa na Chama na Serikali, na la pili likakatiliwa. Linalohitaji maelezo ni hilo la pili
Waingereza wana msemo: 'Ignorance is bliss; ujinga ni baraka.’
Wako watu wanaodhani kuwa pendekezo la Tume ya Nyalali la kutaka Shirikisho la Serikali Tatu,
linatokana na maoni au matakwa ya watu. Hiyo si kweli hata kidogo. Lakini watu wanaotaka tuamini
kwamba wasemavyo ni kweli si watu waongo, ni wajinga tu, maana nadhani hawajasoma Ripoti ya
Tume ya Nyalali. Hotuba ya Waziri Mkuu na Makamu wa Kwanza wa Rais, ya tarehe 30 Aprili, 1992,
katika Bunge Ia Muungano inaeleza vizuri sana ukweli ulivyo.
Mheshimiwa Spika, mojawapo ya mapendekezo makubwa yaliyotolewa na Tume ya Nyalali lilihusu
mfumo wa Muungano na Ushirikiano kati ya Tanzania, Visiwani. Tume ya Nyalali ilipendekeza
kuubadili mfumo wa Muungano ili kuanzisha mfumo mpya ya Shirikisho lenye Serikali Tatu. Yaani,
Serikali ya Shirikisho, Serikali ya Tanganyika na Serikali ya Zanzibar. .

Mheshimiwa Spika, hili ni pendekezo kubwa na la msingi ambavyo kama ilivyofanya Tume, Chama
Cha Mapinduzi na Serikali zimelitafakari kwa undani zaidi. Katika kufanya hivyo, historia ya
Muungano tangu tarehe 26 Aprili, 1964 hadi sasa imezingatiwa. Muungano kama mnavyofahamu
Waheshimiwa wabunge chimbuko lake ni mapatano ya “Articles of the Union yaliyotiwa sahihi na
waasisi wa Muungano; Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere na Hayati Mzee Abeid
Amani Karume, Mungu aiweke roho yake pema.
Mapatano hayo yalifanywa kwa manufaa ya wananchi wote wa Tanzania. Hilo halina ubishi.
Miungano mingi ya aina hii duniani, imefanywa na viongozi kwa njia hii au nyingine kwa niaba ya
wananchi, bila kuhojiwa na hapana sababu ya kuhojiwa kitendo hicho. Kwa msingi huo wale
wachache wanaohoji na kutaka kura ya maoni juu ya suala hili, hawaitakii mema nchi hii. Hoja
hiyo haikubaliwi na Serikali ya Chama Cha Mapinduzi. (Makofi) Mheshimiwa Spika, tangu
kuanzishwa kwa Muungano wa nchi zilizokuwa Jamhuri ya watu wa Zanzibar na Jamhuri ya watu wa
Tanganyika, ziliungana na kuwa nchi maja na Taifa moja. Narudia tena, ziliungana kuwa nchi moja na
Taifa moja. Kwa lugha ya kigeni, 'One Sovereign State'. Hivyo imejenga msingi imara wa umoja kati
ya wananchi wa Tanzania. Tanzania Bara na Visiwani, zimekuwa zikifaidika kisiasa, kiuchumi na
kiulinzi chini ya mfumo uliopo waMuungano. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, nakubaliana na baadhi ya sababu zilizotolewa na Tume ya Nyalali kuwa ndizo
ambazo mara nyingine zimesababisha hali ya kutoridhika na mfumo wa Muungano. Matatizo yapo,
mengi ya matatizo hayo ni ya utekelezaji yaliyojitokeza wakati wa kushughulikia mambo ya
Muungano. Na bila ya kuyaficha baadhi ya matatizo hayo ni mambo yanayohusu suala la uraia, milki
ya fedha za kigeni, ukusanyaji na mgawanyo wa maapato kurokana na kodi na ushuru wa forodha,
tatizo la formula ya kuchangia gharama za Muungano n.k. Hakuna shaka kwamba haya ni matatizo na
mara nyingine yanakera.
Hata hivyo, kwa heshima zote kwa Tume Waheshimiwa Wabunge watakubaliana nami kuwa utatuzi au
ufumbuzi wa matatizohayo, hautapatikana kwa kuanzishwa Shirikisho la Serikali tatu. Kinyume chake
hiyo itakuwa ni chanzo cha kufifia umoja na mshikamano wa Tanzania uliojengeka tangu mwaka 1964.
Inatoa mwanya kwa wasiopenda umoja huo hatimaye kuuvunja. Hiyo siyo kwa manufaa ya wananchi
wa Tanzania nzima. (Makofi) Mheshimiwa Spika, matatizo ni lazima yatatuliwe. Hivyo ni azma ya
Chama Cha Mapinduzi na Serikali kuelekeza nguvu zake zote katika kutafuta ufumbuzi wa matatizo am
bayo. Serikali na Chama zitaendelea kutafuta ufumbuzi wa matatizo bayo halisi na kuyaondoa kwa
manufaa ya wananchi wote wa Tanzania chini ya mfumo wa sasa. Hivyo kwa sasa Serikali inaifanyia
kazi maeneo yanayohusika. Uhusiano wa Serikali ya Muungano na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar na
hasa katika maeneo yanayohusu matatizo niliyoyaainisha.
Kwa mtazamno huo, ndiyo maana katika marekebisho ya Katiba wakati huo, eneo linalohusu Rais wa
Jamhuri ya Muungano pamoja na uchaguzi wake na wa Makamu wake ambaye pia ni Rais wa
Zanzibar linawekwa kando, likisubiri mapendekezo mapya ya Serikali kwa Bunge lako Tukufu kwa
kutungiwa muswada utakaowasilishwa hapo baadaye katika Bunge lako Tukufu.
Kwa wakati huu sehemu hii ya katiba itatoshelezwa kwa muda na ibara ya 37 ya katiba ya Jamhuri.
Rekebisho hili limefanywa katika Muswada na kubadili katika katiba.
Mheshimiwa Spika, kwa kuzingatia ukweli kwamba tangu mwanzo ulipoanzishwa Muungano Waasisi
kwa makusudi kabisa hawakutuachia muundo wa Shirikisho la Serikali tatu au Serikali moja, ni
dhahiri muundo unaopendekezwa unatutoa kutoka msingi huo wa awali. Ni mfumo ambao
unadhoofisha nchi nzima ya Tanzania. Kwani Shirikisho ambalo lingeweza kuundwa na nchi mbili
huru zenyewe zikibakia kuwa ni Jamhuri na hivyo kuwa na Serikali tatu. Halitasaidia lolole katika
kudumisha hali ya utulivu na usalama ya wananchi wetu. (Makofi)
Hapatakuwa na. mshikamano madhubuti katika masuala ya uchumi na maendeleo ya jamii na
gharama ya kuziendesha Serikali tatu, ingekuwa kubwa sana na isiyo ya lazima. Kwa sababu hizi,
ndiyo maana Chama Cha Mapinduzi na Serikali yake hazikubali pendekezo la Tume ya Nyalali la
kuanzisha mfumo mwingine wa Muungano wa Serikali tatu. (Makofi).
Isitoshe Mheshimiwa Spika, hata pendekezo hili silo la wananchi wengi. Kwani taarifa ya Tume
inasema, na naomba ni nukuu. "Zaidi ya hayo wengi wa wananchi waliotoa maoni yao kwa Tume
hawakuelezea chochote juu ya mfumo wa Serikali ambao Muungano uwe nao.
Kati ya wananchi elfu tatu (3,000) waliojitokeza kwenye Tume huko Zanzibar ni wanne (4) tu
waliozungumzia jambo hilo ambayo ni asilimia (0.13) ndio waliopendekeza kuwepo kwa mfumo wa
Serikali tatu. Na kati ya wananchi 32,275 waliotoa maoni yao kwa Tume ndio waliopendekeza mfumo
wa Serikali tatu.
Wana-Tume ambao hawakubaliani na pendekezo hilo la kuwa na Serikali tatu,
walisisitiza kwamba na ningewanukuu; "Pamoja na kuelewa kuwa baadhi ya mambo mengine siyo
lazima uamuzi wake; kutegemea wingi wa watoa maoni lakini pia tunaona kuwa siyo busara
kupendekeza mabadiliko makubwa kama haya ya mfumo wa Muungano wetu kwa kutegemea maoni ya
Watanzania 49 kati ya Watanzania 36,299 walioshiriki katika mjadala wote, ulioendeshwa na Tume ya
Rais. Idadi hii ni ndogo isiyo na uzito kitakwimu."
Sisi hatuoni kuwa kuna hoja ya kisheria na ya kisiasa ya kubadili mfumo wa sasa wa Serikali mbili na
kuanzisha mfumo wa Serikali tatu. Tunaamini kuwa mfumo wa Serikali tatu, utadhoofisha
Muungano wetu kisiasa na kiuchumi". (Makofi).
ITAENDELEA..................USIKOSE